JE HAYA NI MAPENZI!! 106:



Wakiwa kwenye staili ile, mlango wa kuingilia
sebleni ulifunguliwa na aliyeingia alikuwa ni Sam.
Na mbele yao alitokea mama yake Sabrina kutoka
chumbani kwake, kwahiyo macho ya mama
Sabrina na macho ya Sam yalikutana katika
kumshangaa Jeff na Sabrina.
Macho ya mama Sabrina yaliwashtua sana Sabrina na Jeff kwani ndio alikuwa upande wao, Sabrina alijiondoa haraka kwenye mikono ya Jeff ambaye alikuwa kwenye harakati za kumbusu.
Sabrina alivyojiondoa kwenye mikono ya Jeff ndipo alipogeuka nyuma ili ayakwepe macho ya mama yake ila hapo akagongana na macho ya Sam na kujikuta akikumbuka neno la mwisho la Sam kuwa anahitaji kuheshimiwa.
Aibu ikamjaa zaidi Sabrina na kujikuta akimfata Sam kama kuhitaji kumkaribisha ili kujigelesha na kuiondoka aibu ile ingawa imesha mfedhehesha.
"Karibu Sam"
Sam alimuangalia Sabrina na kutikisa kichwa kama ishara ya kusikitika.
Mama Sabrina nae akaona wazi kuwa kitendo cha yeye kuendelea kuwa hapo na kushangaa kitazidi kumkasirisha Sam, hivyo akajifanya kamavile hakuona na kuelekea jikoni.
Jeff alikuwa kasimama pale pale huku akiogopa hata kugeuka na kumtazama Sam ambapo akaisikia sauti ya Sam ikisema kwa taratibu kabisa,
"Umeshinda Jeff, mtoto mdogo lakini umenishinda akili"
Jeff alikuwa kimya kabisa kwani hata uoga ulianza kumjaa na kutamani hata kurudisha masaa nyuma.
Ile hali aliyokuwa nayo Jeff, Sam aliielewa vizuri sana.
Akamfata na kumshika mkono kisha akatoka naye nje, kitendo hicho kilimpa mashaka Sabrina na kuamua kuwafata ili kuona kitakachoendelea.
Ila Sam alipofika na Jeff nje akamwambia,
"Nenda nyumbani, ila kesho njoo unisindikize na mke wangu tukielekea nyumbani kwetu"
Jeff alitikisa kichwa tu kwani uoga aliokuwa nao kwa muda huo ulikuwa wa hali ya juu.
Kisha akaondoka huku akiwa haamini kama ameweza kuondoka salama.

Sabrina alipoona kuwa Jeff kaondoka ndipo na yeye aliporudi ndani huku Sam akiwa nyuma yake ambapo alimuuliza swali kwa sauti ya chini tu.
"Wakati naondoka nilikwambiaje Sabrina?"
Sabrina alikuwa kimya kanakwamba hajasikia swali aliloulizwa na Sam ambapo walifika pale sebleni kisha Sabrina akakaa na Sam nae akakaa ambapo akamwambia tena,
"Kesho tutarudi nyumbani."
Sabrina bado akajifanya hajasikia na kuamua kumuuliza swali lingine Sam,
"Kwani na leo unalala hapa hapa?"
Sam akatabasamu tu kwani alijua wazi kuwa Sabrina anakwepa kile ambacho alikisema na kuamua kumuitikia tu kuwa atalala pale pale.
"Basi ngoja nikakuandalie kile chumba cha jana"
Sabrina aliinuka na kwenda kuandaa chumba hicho.
Muda mfupi tu akatoka tena mama Sabrina na kumfata Sam pale kwenye kochi na kumwambia,
"Samahani mwanangu kwa yaliyotokea"
"Usijali mama"
"Ushaingiza gari yako ndani? Kama bado twende nikakufungulie geti uingize"
Kisha Sam akainuka na kuelekea nje ili aweze kuingiza gari.

Jeff aliingia kwao na kumkuta mama yake pale sebleni ila alisahau kumsalimia tena na kupitiliza chumbani.
Sakina akahisi kuwa lazima kuna kitu kwa mwanae kwani ile hali haikuwa ya kawaida. Na akajua tu kuwa ni ni lazima hicho kitu kipo huko alipotoka Jeff kwa wakati huo na kwa haraka haraka akahisi tu lazima atakuwa ametoka kwakina Sabrina hivyo akaamua kuinuka na kwenda kwakina Sabrina ili kuchungulia kuwa kuna kitu gani kilichotokea.
Alifika karibia na kwakina Sabrina na kuona kuna gari ikiingia ndani na kuigundua kuwa ile ni gari ya Sam.
Akatamani kwenda kuulizia ila akajiona kuwa ataonekana ni mmbea sana na kuamua kurudi nyumbani kwake ila alipofika tu akamuita mwanae Jeff ambaye alitoka pale sebleni na kumsikiliza mama yake,
"Una matatizo gani kwani mwanangu?"
"Kwanini mama?"
"Mbona ulipita hapa bila hata ya kunisalimia halafu akili yako inaonyesha kuwa haupo sawa kabisa"
"Nisamehe kwa kutokukusalimia mama ila nipo kawaida tu kwani sina tatizo lolote mama"
"Haya na leo kutwa nzima ulikuwa wapi toka asubuhi ile?"
"Kheee mama jamani ndio unanifukuza hapa nyumbani au? Nina mengi ya kuzungumza na wewe  yangu ila yapo ya muhimu zaidi nitakwambia ila kesho"
"Hapana, naomba uniambie muda huu huu. Unajua watu kama sisi tukiambia kuna kitu cha kuambiwa huwa hatupendi kusubiri tafadhari sana niambie leo leo tena muda huu"
Jeff akacheka kidogo kwani alimtambua vizuri mama yake kuwa ukimwambia kitu si mtu wa kusema kuwa asubirie yani yeye hupenda kuambiwa hapo hapo ingawa mara nyingine humfanyia ngumu ya kutokumwambia.
Ila leo aliamua kumdokezea tu kwa yale aliyoambiwa kuhusu baba yake,
"Kwahiyo umeacha kufanya kazi zako ukaanza kufatilia kuwa baba yako alipatwa na nini!"
"Sio hivyo mama, hii khabari imekuja tu bila hata mi kuihitaji ila nimeona wazi kuwa itakuwa na umuhimu sana katika maisha yangu na yetu pia"
Kisha Jeff akamwambia mama yake jinsi alivyoelezwa kukutana kwa mama yake na baba yake ila kabla hajamalizia mama yake aliinuka na kwenda chumbani.

Sakina alionekana kushikwa na uchungu sana kwani kule  chumbani alienda kukaa na kujiinamia huku machozi yakimtoka kwa mfululizo kwani alikumbuka alivyokuwa akiishi na mumewe, mambo yaliyotokea na mpaka mwisho wa siku kutokomea kabisa kwenye macho yake na macho ya mwanae. Kwa muda huo alikuwa na maumivu sana ila alimsikia mwanae akimgongea mlango na kumfanya afikirie sana na kuona kuwa mwanae hana makosa na anatakiwa kujua ukweli wa mambo yote ukizingatia kwasasa mwanae ameshakuwa mtu mzima.
Moyo wa huruma dhidi ya mwanae ukajaa na kuamua kwenda kufungua mlango ili akaendelee kuzungumza na mwanae,
"Nisamehe mwanangu."
"Usijali mama naelewa, na pole sana mama yangu"
Sakina alimuangalia mwanae kisha akaenda naye sebleni ili wakae na waweze kuzungumza.
Sakina alianza kwa kumwambia mwanae,
"Sikia Jeff mwanangu nikwambie kitu kuhusu mi na baba yako, yani haya mapenzi haya wee yaache tu"
"Kwani mama wewe na baba si mlikuwa mnapendana lakini?"
"Kupendana ndio, lakini kupendana kwetu ni kulitengenezwa"
"Kivipi mama?"
Jeff alikuwa makini sana kumsikiliza mama yake,
"Kabla ya mimi kuwa na baba yako, alikuwepo kijana mmoja ambaye alinipenda sana na hata mimi nikampenda. Tatizo kwa yule kijana ni kuwa alikuwa masikini kipindi hicho, hakuwa na uwezo hivyobasi kwetu hawakumkubali kabisa na kunitafutia kijana mwingine ambaye ndio huyo baba yako. Kwa kipindi hicho alionekana kuwa na nia sana ya kuoa na ndipo aliponiona na nikaja kuishi nae mjini. Maisha yalikuwa mazuri sana kabla ya lile lishetani kuingilia mapenzi yetu. Nimefanya kila jitihada za kuweza kumrudisha baba yako kwenye mstari lakini juhudi zangu zimegonga mwamba kwani ndio kwanza yametokea mashetani makubwa zaidi na kumtokomeza baba yako. Kwakweli huwa naumia sana nikimfikiria, tungekuwa tunafurahia maisha yetu ila ndio hivyo kaniachia wewe tu"
"Pole sana mama, ila Mungu ni mwema. Tumuombee tu baba kuna siku atatukumbuka familia yake"
"Hata mi naamini hivyo mwanangu"
"Ila mama huyo aliyekuwa akikupenda zamani yuko wapi siku hizi?"
"Yani maisha haya yaache tu huwa hayatabiriki, saivi ana maisha yake mke na watoto. Ni mfanyabiashara mkubwa sana huwezi hata kufikiria kuwa ni yeye, roho huwa inaniuma sana najutia kwa kusikiliza maneno ya watu kuwa nitakufa masikini nikiwa na yule mwanaume ona sasa hapa nilipo hata sijielewi"
"Ila je huyo mtu bado unampenda mama? Na vipi yeye bado anakupenda?"
"Hayo maswali sitaki, hebu tukalale kwanza"
Sakina aliyasema hayo huku akitabasamu na akionekana kama kujifuta tu machozi, hivyo Jeff akaamua kumuaga tu mama yake kisha yeye kuelekea chumbani kwake kwani alijua wazi kuwa kuendelea kuzungumza nae ni kuzidi kumpa uchungu.

Jeff alipoingia chumbani kwake alienda kukaa kitandani na kujikuta akitafakari maneno ya mama yake na kuwaza jinsi maneno ya watu yanavyovunja  mahusiano,
"Ila kwakweli mimi nina haki yote ya kuwa na Sabrina kwanza nampenda halafu na yeye ananipenda, pili bila ya mimi pengine Sabrina angeshakuwa marehemu kwa siku nyingi sana. Ingawa Sabrina ni mkubwa kwangu ila mimi ndio nimeshampenda, na kama ingekuwa ni hairuhusiwi kwa kijana mdogo kumpenda mdada basi ingekuwa ngumu kwa mimi kumpenda Sabrina. Ila hadi nimempenda na kumuacha siwezi basi ni wazi kwamba Mungu aliniandikia kuwa niwe nae. Haya mengine ni mapito ya muda tu kwani najua kuwa ipo siku Sam atagundua jinsi upendo wangu ulivyo kwa Sabrina ni zaidi ya upendo wake. Kwakweli nampenda sana Sabrina na ni Mungu pekee ndiye anayetambua upendo wangu kwa huyu dada"
Jeff alijifikiria sana na akawaza pia jinsi atakavyokutana na Sam kesho yake na kama atamuuliza tena kuhusu alichokuwa anafanya na Sabrina, ni hapo ambapo moyo wake ukaghairi kwenda kuwasindikiza wakina Sam kwa siku hiyo ya kesho.
 
Sam alipoamka asubuhi alitoka sebleni na kumkuta Sabrina nae akiwa tayari pale sebleni na kumuomba kuwa aanze kujiandaa ili warudi kwenye nyumba yao.
Hata mama Sabrina alipotoka ndani, Sam alimpa hoja hiyo hiyo.
"Ila mwanangu mbona mapema sana? Hata baba yenu sijamwambia kuhusu hili."
"Ila mama, kumbuka kwamba Sabrina ni mke wangu na pia nina uwezo wa kulea watoto ninao sasa kwanini nisiichukue familia yangu?"
"Lakini kumbuka kuwa baba Sabrina alishakataa hilo swala"
"Naelewa mama ila kutenda kosa si kosa bali kurudia kosa, najutia makosa niliyoyafanya hapo awali ila kwasasa naomba nipe ruhusa tu nikaendelee kuishi na mke wangu"
Mama Sabrina alijitahidi kumuomba Sam kuwa amuache Sabrina pale ila Sam hakukubali na kuendelea na hoja zake ambazo kweli zilikuwa za msingi na kumfanya mama Sabrina kuwaruhusu tu.
Ila kabla ya kuondoka akamvuta mwanae pembeni na kuzungumza nae kidogo,
"Kwakweli kile kitendo  kilichotokea jana usiku baina yako wewe na Jeff sijakipenda, tena sijakipenda kabisa. Sabrina mwanangu hebu jaribu kufikiria kuwa una watoto na kubwa zaidi una mume. Halafu jambo lingine ni kuwa sijaona mantiki ya wewe kuwa karibu na Jeff kiasi hicho na hata ile simama yenu ya jana na mabusu yenu sikuyaelewa kwakweli. Tafadhari Sabrina mwanangu usitake kuniaibisha mama yako, utanitia aibu jamani. Yule Jeff ni kama mdogo wako au mwanao, haendani kabisa na wewe. Hebu kaache kale katoto kakawe na watoto wenzie, usinitie aibu jamani"
Sabrina alikuwa ameinama tu akiangalia chini ila maneno ya mama yake yalimuingia vizuri ingawa mama Sabrina aliona kamavile hasikilizwi na kuamua kumuuliza,
"Hivi unanielewa kweli Sabrina?"
"Nakuelewa mama ila usinifikirie vibaya"
"Nisikufikirie vibaya vipi wakati mambo nayaona wazi! Sabrina watoto wako bado wadogo, tulia ulee watoto na mumeo acha tabia za kuruka ruka. Nilikuwa nakuamini sana na wala sikuwa na shaka nikikuona na Jeff ila jana umenipa mashaka kwakweli. Kuwa makini Sabrina tunza ndoa yako"
Mama Sabrina alimaliza hapo kumpa mwanae semina fupi ya kuhusu ndoa.

Sabrina alirudi alipo Sam na kumtaarifu kuwa tayari waende ila mama Sabrina hakuweza kuwaruhusu kuondoka na watoto wote kwa siku hiyo, hivyobasi wakaondoka na yule mdogo sana.
Wakati wanaondoka Sam akakumbuka kuhusu Jeff na kumwambia Sabrina kuwa wakampitie Jeff kwanza,
"Kwanini tumpitie Jeff jamani si twende tu"
"Hapana Sabrina, kumbuna niliwaambia jana kuwa kuna mambo napenda tuzungumze. Nadhani ni vyema kama mambo hayo tukienda kuzungumza nyumbani kwangu ndiomana nataka twende na Jeff"
Sabrina hakuwa na pingamizi na ukizingatia kuwa dereva mwenyewe ndio huyo huyo Sam basi wakaamua kumfata huyo Jeff ambapo ni Sam mwenyewe aliyeshuka kwenda kumuita.

Jeff alitoka ndani na kumuona Sam,
"Vipi wewe Jeff, hapa tumekufata wewe kwani jana nilikwambiaje? Twende basi."
Jeff alijigelesha kidogo ila badae akakubali kutokana na ushawishi wa Sam, kisha safari ya kuelekea kwa Sam ikaanza.

Walifika nyumbani kwa Sam kisha Sam akawaambia kuwa na chakula kitakuja hapo kwani alishatoa oda hotelini.
Kwavile mtoto alikuwa amelala ikambidi Sabrina akamlaze kisha yeye kurudi sebleni ambako Sam alianza kuongea,
"Ni kipindi kirefu sana kwa mimi kuishi na mke wangu ila mke jina"
Jeff na Sabrina wakatazamana tu, kisha Sam akamuangalia Jeff na kusema,
"Jeff mbona umekaa mbali sana, hebu sogea hapa karibu na Sabrina"
Kisha Jeff akasogea na Sam akaendelea kuongea,
"Najua nyie wawili mnapendana sana, ila nataka mnifanyie kitu kimoja tu ili nijiridhishe na upendo wenu"
Sabrina alikuwa wa kwanza kushangaa haya maneno na alikuwa wa kwanza kuuliza,
"Kivipi?"
Sam akacheka na kusema,
"Kumbe kweli mnapendana, sasa chagueni nyie cha kufanya muda huu ili nijiridhishe dhidi ya upendo wenu"
Jeff na Sabrina wakatazamana tena kwani hakuna aliyejua cha kufanya.
Sam akawashtua sasa na kusema,
"Nyie watu, sitaki masikhara mjue! Fanyeni chochote mnachojua kabla sijawachagulia mimi cha kufanya"
Kisha Sam akatoa bastora yake na kufanya uoga uwashike.

Itaendelea







USISAHAU KU LIKE PAGE YETU,BONYEZA LIKE BUTTON

No comments:

Theme images by pollux. Powered by Blogger.