JE HAYA NI MAPENZI!! 109:





"Eeh Sam niambie basi kuwa kwanini uliamua
kuwa kimapenzi na mimi hadi kunioa ingawa
ulijijua kuwa unamatatizo? Na kama ulikuwa na nia
ya kunimaliza mimi kama hao wengine kwanini
hukufanya hivyo kwangu na kuwamalizia wakina
Neema? Na kwanini....."
Kabla Sabrina hajauliza walisikia kamavile nyumba
ikitetemeka na kumfanya Sam naye amuulize
Sabrina kwa hasira,
"Kwanini umemtaja Neema......"
Nyumba ikazidi kuwa na tetemeko na kuwafanya
wapate kizungu zungu ndani.
Tetemeko lile lilifanyika kwa dakikaz kama tano ila liliwasumbua sana kwani walishindwa hata kusimama na kubaki pale pale wakitingishika na kupepesuka kila walipotaka kusimama.
Hali ilipotulia wakajikuta wakitazamana, Sam akahamaki kwa nguvu,
"Ndiomana sipendagi mambo ya waganga kwa sababu waongo, ona sasa kilichotokea"
Sabrina nae akauliza,
"Sasa tufanyaje? Tutoke?"
Kabla Sam hajajibu kuna mtu aliwagongea mlango ikabidi Sam ainuke kumfungulia, alikuwa ni mlinzi wake.
"Vipi Omary, kuna tatizo?"
"Sio tatizo sana bosi ila kuna yule mzee wa siku ile amekuja tena, yupo nje anakusubiri"
Sam akafikiri kwa haraka na kujua kuwa ni lazima atakuwa ni yule mganga wa kienyeji na kwa haraka zaidi akawaza kuwa huenda anahusika na kilichotokea muda mfupi uliopita.
Sam akamuuliza tena mlinzi wake,
"Yupi huyo? Yukoje?"
Mlinzi akamueleza Sam jinsi alivyo yule mzee na kumfanya Sam kuelewa  vizuri kuwa ndio huyo huyo mzee anayemuongelea yeye.
Akageuka na kumuangalia  Sabrina kisha akamwambia,
"Unaona sasa, huyu mganga nae kashafanya kitega uchumi chake hapa. Anafanya mambo ili badae aseme kuwa anataka kutusaidia. Eti yupo nje"
Sabrina nae akajibu,
"Si huwa anauwezo wa kuingia ndani kimiujiza, sasa leo kwanini akuite nje? Mwambie aingie tu."
"Ila kweli Sabrina"
Kisha Sam akamuangalia yule mlinzi wake na kumwambia kuwa amwambie yule mzee aingie tu.
Yule mlinzi nae akawauliza,
"Hivi waganga mnawajua vizuri au? Wanaweza fanya chochote usipofata wanachotaka."
Sam naye akamjibu,
"Omary hata usijali, mi waganga nawajua sana kupita unavyofikiria na ndiomana nimekwambia mwambie aje mwenyewe tu"
Ikabidi yule mlinzi atoke na kwenda kumueleza yule mganga pale nje.

Jeff pale kwao akafikiria sana, akaifikiria ile barua iliyoachwa na Neema na kujua wazi kuwa Sam yupo kumpa maelezo Sabrina kuhusu ile barua,
"Na vipi kama Sam akiamua kufanya na Sabrina kile alichofanya na Neema hadi kudhurika mmh!"
Aliwaza kuwa Sam anaweza kumfanyia Sabrina kama adhabu ya kumsaliti ndio pale alipopata wazo la kurudi tena kwa Sam na kusema kuwa anatakiwa kujikaza kama mwanaume na aweze kukabiliana na chochote kile.
Kisha akaondoka pale kwao akiwa amejipanga vilivyo sasa.
Ingawa alijua hadi kufika tena kwa Sam muda nao utakuwa umeenda sana.

Yule mlinzi wa Sam alienda kumwambia yule mzee kuwa aingie ndani,
"Wameniruhusu wenyewe?"
"Ndio bosi mwenyewe kasema uingie"
Yule mganga akaingia hadi alipofika mlangoni na kuona kuwa mlango umefungwa na kwa maadili yake ya muda huo hakutakiwa kugonga ikabidi atoke nje na kumwambia yule mlinzi wa Sam,
"Huyu bosi wako kajifanya mjanja eeh! Mwache hanijui vizuri na nitamuonyesha kuwa mimi ni nani"
Kisha yule mzee akaondoka hata yule mlinzi wa Sam hakuona kama ni vyema kwa yeye  kubaki na jambo lile moyoni kwahiyo akarudi tena na kuwagongea wakina Sam kisha akawataarifu alichosema yule mganga, Sam naye akajibu
"Kwakweli wasitake kunichanganya jamani, tena mi nilimuheshimu tu siku ile mtu gani yeye kazi kuharibu tu watu hata wasiotaka huduma zake. Mi na Sabrina tumeteseka kumbe chanzo ni yeye, nilimuheshimu sana siku ile na waniache tu nipumzike kwasasa"
Sabrina nae akachangia,
"Amelbniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu"
"Na kweli, sasa hawa waganga wanataka kunizidishia laana tu. Kama siku zingine aliweza kuingia kwangu bila tatizo lolote kwanini leo ashindwe? Simjui kweli yakinizidia nitamtafuta"
Kisha akamwambia mlinzi wake akaendelee na kazi yake.
Walitulia na Sabrina pale huku wakimjadili yule mganga na kuepuka kutaja jina la Neema,
"Sasa mahali ikitulazimu kutaja jina lake tusemeje?"
"Tuseme tu yule mtu maana hilo jina litatuletea balaa bure na hivi umekataa kumfata huyo mzee ndio tutazidisha balaa zaidi bure."
Sabrina aliongea na kufanya wakubaliane kuwa watasema tu yule mtu bila ya kutaja jina.
"Basi jibu maswali yangu Sam"
"Nitakujibu tu Sabrina ila acha kwanza moyo wangu utulie"
Wakakaa pale na muda kidogo Sabrina akamsikia mtoto akilia na kwenda kumchukua ili aweze kumnyonyesha.
Alipotaka kumnyonyesha akashangaa kuona kuwa maziwa hayatoki,
"Sam, eti maziwa hayatoki"
Mtoto nae alizidi kulia kwavile hakupata haki yake,
"Kwanini hayatoki sasa?"
"Hata sielewi, hebu ona!"
Sabrina akajaribu kutoa ziwa na kukamua ambapo hayakutoka maziwa kabisa wala chochote,
"Khee mbona makubwa haya leo, yani maziwa yangu hayatoki kabisa wakati yanatokaga mengi sana"
"Sasa ndio nini hiki jamani? Kitu gani hiki"
"Labda yule mganga wako kaamua kunifanyia vipi"
Wakatazamana bila kujua cha kufanya kwa haraka na mtoto naye aliendelea kulia tu.
Ikabidi Sam atoke akaangalie japo maziwa ya   ziada waweze kumpatia mtoto.

Sabrina alibaki mwenyewe akimbembeleza mtoto kwa kila staili.
Muda kidogo Sam akawa amerudi na maziwa ya unga kwa watoto, Sabrina akamkorogea mtoto na kuanza kumnywesha ambapo alikuwa kidogo na kuyakataa kisha kilio kikaongezeka zaidi.
"Huyu mtoto naye mbona shida eti kayakataa maziwa tena"
"Sasa tufanyaje?"
"Twende hospitali tukamueleze daktari labda anaweza kutusaidia"
"Sabrina, huu ni ushirikina unafanyika hapa hata hospitali hatutasaidika"
"Sasa unafikiri Sam tutafanyaje na mtoto analia kiasi hiki?"
Hawakujua cha kufanya ila tu walikuwa wakimbembeleza mtoto anywe yale maziwa.

Jeff naye alipofika akashangazwa na sauti ya kilio kwa mtoto na moja kwa moja alifika na kuingia ndani kwani muda huu Sam hakufunga kama mwanzo.
Naye alianza kwa kuwauliza kuwa ni kitu gani kimetokea mpaka imekuwa vile, ikabidi Sam amueleze kwa kifupi tu kuhusu ujio wa yule mganga na jinsi   Sabrina alivyojikuta kuwa maziwa hayatoki kwa muda huo na mtoto anavyokataa maziwa waliyomletea.
"Mmh huu ni ushirikina tu"
"Ndio hata mi nimemwambia Sabrina hivyo ingawa anang'ang'ania kuwa twende hospitali."
Jeff akamkumbuka hapo hapo yule daktari aliyesaidia hadi Sabrina kujifungua salama kabisa na kuwaeleza kuwa kwanini wasiende huko kwani aliona yule daktari kuwa na uwezo mkubwa zaidi ingawa hakumueleza wazi Sam kuwa ni kitu gani kilitokea siku ya kujifungua kwa Sabrina.
Basi wakapanda kwenye gari kisha safari ya kuelekea huko hospitali ikafanyika.
Mtoto alilia na mwisho wa siku akalala tena na kutulia.
"Mmh bora amelala jamani maana si kwa kilio hiki wapendwa."
"Mambo yatakuwa sawa tu, najua hukumbuki Sabrina ila yule daktari ana utambuzi wa hali ya juu jamani yani hata kama mtu wamekuchezea yeye anajua kwahiyo atagundua haraka kuhusu huyu mtoto na atatuambia kitu sahihi cha kufanya"
Waliongea huku safari ya kwenda hospitali ikiendelea hadi pale walipofika.

Waliingia hospitali na kwenda moja kwa moja kwa daktari aliyemtibia Sabrina kwa maelekezo ya Jeff kwani ndiye pekee aliyejua kisa na mkasa wa Sabrina wakati wa kujifungua.
Walimkuta yule daktari akiwa ofisini kwake huku akiendelea na mambo yake ya kuandika andika.
Yule daktari naye alipowaona tu akamkumbuka Jeff na kumuuliza,
"Vipi tena kijana, mkeo kapatwa na tatizo gani?"
Sam akamtazama Jeff kwa kujijulisha vile kuwa yeye ni mume wa Sabrina wakati mume halali ni yeye.
Jeff alitambua hilo ila kwavile alihitaji kuangalia hali ya maisha ikabidi amjibu dokta vile inavyotakiwa,
"Kuna tatizo daktari, mke wangu hatokwi na maziwa"
"Na mbona mmekuja watatu ofisini?"
"Huyu ni bosi wetu na anajua kila kitu kuhusu sisi ndiomana tumekuja nae"
Huku akimuonyeshea Sam na kumfanya Sam azidi kujisikia vibaya ingawa yule daktari aliwaambia wakae ili ampime Sabrina ila kabla hajampima akasita kidogo na kuwaomba wampatie mtoto kwanza.
Sabrina akamkabidhi yule daktari mtoto ambapo daktari alimshika mtoto huku akitikisa kichwa na kuuliza,
"Hivi kwanini mtu kutaka kumtesa malaika kama huyu? Huyu ni mtoto mdogo sana, watu hawajui tu kama watoto wanalindwa na Mungu. Mlitaka kumpa maziwa huyu mtoto ila yakawekwa uchafu gafla na akayakataa"
Sam akamuangalia Sabrina kwani kweli walimpa maziwa mtoto ambapo aliyakataa maziwa hayo.
Huyu daktari naye akawatazama kanakwamba akihitaji uthibitisho kwa kile alichokisema, naye Sabrina akaitikia kuwa ni kweli ilikuwa hivyo.
Daktari akamtazama Sabrina, kisha akamtazama Jeff na kusema,
"Hili si tatizo kubwa kama ambavyo mtengenezaji analifikiria kuwa ni kuwa ila litakuwa ni dogo endapo utakuwa na imani. Najua wewe kijana unanishangaa sana, ukweli ni kwamba mimi nisingekuwa nimesoma basi ningekuwa mganga wa kienyeji au  kama ningeshika sana dini basi ningekuwa nabii. Ninachoweza kufanya huwa nasema naweza na ninachoshindwa huwa natoa angalizo kabisa kuwa nimeshindwa. Kwa kusema haya ni hivi, siwezi kumtibu mtoto huyu wala mama huyu kwa dawa yoyote hapa"
Ile kauli ikawashtua kidogo na kuwafanya watazamane huku wakifikiria cha kufanya ili Sabrina na mtoto wawe huru.
"Sasa tutafanyaje daktari?"
Sam aliuliza kwa mshangao kidogo.
"Msijali, cha kufanya ni imani tu"
Kisha akamuangalia Jeff na kumuuliza,
"Je, una imani?"
"Ndio imani ninayo"
"Basi inuka, shika matiti ya mkeo na uyaamuru yatoe maziwa huku ukiamini kuwa Mungu atatenda hilo"
Jeff akainuka na kufanya kama daktari alivyomwelekeza kisha akakaa.
Daktari akawapa mtoto na kuwaambia,
"Haya nendeni, tatizo lake limeisha"
Walimchukua mtoto na kuondoka kama kwa mashaka hivi yani kama vile hawaelewi kinachoendelea hadi walipopanda kwenye gari na Sam akawa wa kwanza kuuliza,
"Hivi huyu daktari mmemuelewa jamani?"
"Hata sijamuelewa"
"Haya tuachane na hayo, eeh Jeff na Sabrina inamaana ndio mmeshajihalalisha na huku kuwa nyie ni mke na mume?"
Jeff na Sabrina wakatazamana, na wala Sabrina hakuwa na jibu ukizingatia hakujua chochote kilichotokea wakati wa ugonjwa wake ndipo Jeff alipoamua kueleza ukweli wa kilichotokea huku akiwaomba msamaha.
"Huna haja ya kuomba msamaha Jeff kwani mambo yapo wazi kabisa kuwa huyo mtoto kwa Sabrina ni wako ingawa sitaki hata kufikiria kuwa ilikuwaje kuwaje hadi ikawa hivyo aaarghh"
Mtoto naye akaamka na kuanza kulia tena, Sabrina akampa ziwa na muda huu maziwa yalikuwa yakitoka vizuri sana na kumfanya Sabrina afurahie,
"Eti maziwa yanatoka"
Sam alijibu kwa haraka sana,
"Lazima yatoke si yameshikwa na mwizi bhana"
Sabrina akawa kimya na Jeff naye akawa kimya kabisa huku wakitazamana kwa aibu.

Sam alipeleka gari hadi nyumbani kwake na muda nao  ukawa umeenda tayari.
Walifika na kuingia tena ndani huku Sam akionekana kuwa na mawazo sana.
Walikaa sebleni ila Sam aliinama kuonyesha kuwa bado kuna kitu anafikiria sana.
Alijiuliza kuwa kwanini hawezi kumdhuru Jeff, hata kama ni sababu ya kumpenda Sabrina ila bado haikuwa sababu tosha ya kumfanya yeye ashindwe kumdhuru Jeff.
Akajikuta akiinua kichwa na kuongea kwa nguvu,
"Hivi wewe mtoto una nini wewe?"
Jeff naye alimtazama tu Sam bila ya kusema chochote na kumfanya Sam amuulize tena,
"Hivi wewe Jeff una nini lakini? Unajua sikuelewi!"
Kisha akamuangalia na Sabrina halafu akauliza,
"Ni kweli alikubaka au kwa mapenzi yako tu ukaamua kulala naye? Hivi Sabrina unajijua kwamba wewe ndio tiba yangu? Hivi unajua kwamba wewe ndio ulitakiwa kunitoa kwenye hili janga? Badala yake ukaharibu masharti yote kwa kwenda kulala na huyu mtoto. Hivi mi niwafanyeje lakini"
Sabrina alimuangalia Sam na kusema,
"Mbona sikuelewi Sam, umepatwa na nini tena gafla?"
"Roho inaniuma mjue, tena nikifikiria kuwa kijana mdogo kama Jeff wa kunipiku mimi kweli? Na pesa zote nilizonazo kweli?"
Sabrina akaona itakuwa shida na kuamua kuinuka ili akamlaze mtoto kwanza ila alipofika chumbani akashangaa alichokiona na kuamua kuwaita Sam na Jeff nao walishangaa walichokiona kwani walimuona mtoto mwingine mdogo kama mtoto wao akiwa amelala kitandani.

Itaendelea







USISAHAU KU LIKE PAGE YETU,BONYEZA LIKE BUTTON

No comments:

Theme images by pollux. Powered by Blogger.