JE HAYA NI MAPENZI!! 111:



Muda kidogo yule mlinzi wa Sam akasikia mlio wa risasi na kumfanya nae aingie ndani ya geti, akashangaa kumuona yule mzee chini huku damu ikiwa imetapakaa eneo lile.
Sam alikuwa amesimama huku kashikilia silaha yake mkononi, yule mlinzi alimshangaa sana Sam ambapo Sam akaongea kwa ukali,
"Unashangaa nini wewe kwani hujawahi kumuona mtu aliyekufa? Huyu mzee si ndio mchawi mashuhuri basi mi nataka kuona uchawi wake unavyoshindana na kifo."
Yule mlinzi bado akamtazama tu Sam kwani hata uwezo wa kumzuia hakuwa nao.
Sam akamuomba yule mlinzi kusaidiane kumbeba yule mzee kisha wakampakiza kwenye buti ya gari ya Sam ambayo ilikuwa pale ndani.
"Sasa shughuli nimemaliza, Omary nitakupeleka kwenye nyumba yangu nyingine ukalinde huko kwani hii nitaipiga bei."
Mlinzi aliitikia tu kwani hakuwa na namna yoyote ya kumbishia bosi wake huyu.

Sabrina akatoka chumbani ili amchukue mtoto ila alipowakuta pale sebleni Jeff na mama yake ikabidi ajifanye anawashangaa wote wawili.
"Jamani leo vipi mama na mwana kuja mapema mapema?"
"Si kwaajili ya kuwasalimia jamani kwani kuna ubaya?"
"Hakuna ubaya dada yangu"
Kisha Sabrina akamchukua mtoto na kumpeleka chumbani.
Alimlaza na kukaa chini huku akitafakari kidogo kwani alishapatwa na hisia kuwa kuna kitu Sakina atakuwa amekihisi baina yake yeye na Jeff, akajikuta akiongea mwenyewe
"Mapenzi jamani mapenzi kwanini mapenzi? Ni kweli nilikuwa nampenda Jeff ila si kimapenzi kwani nilimpenda kawaida kama mtoto tu. Iweje leo nimpende kimapenzi? Iweje nimpende wakati alinibaka mara ya kwanza? Hivi mapenzi gani haya? Mbona yananichanganya jamani kwani nafikia hatua hata ya kutamani kuishi naye duh mapenzi haya, aliyesema kizunguzungu hata hakukosea."
Mara akafatwa na mama yake na kupewa simu,
"Simu hii ongea nayo amekuulizia wewe"
Sabrina akachukua ile simu na kuanza kuongea nae, akagundua kuwa ni yule mlinzi wa Sam na kuamua kumsikiliza kwa makini sana,
"Hebu jaribu kuwasiliana na bosi maana naona kamavile hatokuwa sawa , mpigie kwa simu yake ile nyingine sababu hii kaiacha ndio nimeamua kuwapigia huko"
Sabrina alimsikiliza kwa makini sana na ikawa ngumu kumuelewa kwani yule mlinzi hakusema kuwa Sam kapatwa na nini zaidi ya kusema anahisi hayupo salama.
Simu ilipokatika, Sabrina akamrudishia mama yake kwani ilikuwa ni simu ya mama yake.
Alichekecha akili yake na kukumbuka kuwa Sam alipoondoka alisema anaenda kwa yule mzee ndipo hapo alipopatwa na mashaka kisha kwenda kumuomba mama yake simu ili ampigie Sam.

Akawasiliana nae ila Sam alionekana kawaida tu kuwa hana tatizo lolote,
"Upo sawa kweli Sam?"
"Nipo sawa ndio, hata usiwe na mashaka"
"Vipi yule mzee ulienda kuonana nae?"
"Tutaongea vizuri nikija hata usijali"
Sam akakata simu na kumfanya Sabrina abakiwe na jibu la njiapanda tu kuwa asijali.
Akamrudishia simu mama yake aliyekuwa sebleni kwa muda huo kisha yeye akarudi chumbani.
Jeff nae na mama yake wakamuaga pale  mama Sabrina na kuondoka zao.
Walipokuwa wanatoka wakapishana na James akiwa na mkewe Joyce pamoja na watoto wao ikabidi nao warudi ndani ili wasalimiane vizuri.
Wakina James walikuwa wamechangamka sana na walionekana kuwa na furaha kwa kipindi hicho baada ya kile kipindi cha mkangaranyiko wa matukio ambao uliwapata.
Mama yao aliwakaribisha vizuri sana na alifurahi sana kuwaona.
Akawachukua wajukuu zake na kuwashika kwa pamoja kwavile alikuwa na furaha sana kwa kile alichokiona mbele yake.
"Karibuni sana jamani, maana najihisi raha kuwaona"
"Tumekaribia mama, tuliwakumbuka sana kwakweli"
Mtoto wa kwanza wa Sabrina baada ya kusikia zile kelele kelele naye akaamka na kutoka pale sebleni, na alipofika tu akawashangaa kwa muda halafu akaenda moja kwa moja alipo Jeff ingawa James naye alimuita ili amsalimie,
"Kheee mama huyu ndio mtoto wa Sabrina?"
"Eeh ndio Cherry huyo"
"Khee amekua huyo hadi raha, ameanza na kuongea tayari?"
"Anaongea makorokocho tu, anaelewana na huyo huyo aliyembeba"
Joy nae akachangai,
"Halafu kafanana nae sana"
Mama Sabrina nae akaongezea,
"Khee mnamshangaa huyo kwavile hamjamuona yule mdogo ndio kafanana nae balaa"
Sakina alikuwa kimya kabisa ila Jeff naye aliishia kutabasamu tu.
Sabrina nae akatoka ndani na kuwakuta na ile mada.
Akawasalimia pale na kuongea mawili matatu ambapo Jeff na mama yake wakaaga tena na kuondoka ila yule mtoto wa Sabrina kama kawaida akaanza kumlilia tena Jeff na kumfanya Sabrina acheke na kusema,
"Hivi wewe mtoto una matatizo au? Umeanza lini kumlilia Jeff!"
Mama Sabrina nae akaongezea,
"Sio leo tu, ni mara kwa mara akija anamlilia"
Sabrina akamchukua mwanae na kumbeba ambapo Joy nae akaongea,
"Nadhani amejua kama anafanana nae ndiomana anamlilia"
Sabrina akaguna tu huku Jeff na mama yake wakitoka na kuwaacha wale ndani wakizungumza.
Sabrina akakaa  chini na kumchukua yule mtoto wa kwanza wa kaka yake na kumpakata pamoja na mwanae kisha akawa kama anachombeza,
"Mbona huyu nae hafanani na baba yake?"
Joy akatulia kwanza na kupooza,
"Kafanana na babu yake huyo"
Sabrina akaguna na kucheka tu, kisha akasema,
"Kweli mtoto sio lazima afanane na baba yake jamani kwani anaweza kufanana na yeyote duniani kutokana na uumbaji wa Mungu"
James hakuchangia hapo wala mama Sabrina hakuchangia zaidi ya Joy kutabasamu tu na kubadilisha mada kwani alijua wazi kuwa mada ile ingeenda ndivyo sivyo.

Jeff na mama yake walitoka kwa kina Sabrina pamoja tena vizuri kabisa ila njiani Jeff akamuaga mama yake kuwa kuna mahali anaenda, Sakina hakuwa na pingamizi zaidi ya kuagana nae tu kisha Jeff akaondoka zake.
Sakina alifika nyumbani na kujitafakarisha sana kwani aliona ni jinsi gani kila mtu anawafananisha watoto wa Sabrina na mwanae Jeff na kumfanya aendelee kupata uhakika wa mawazo yake ingawa hakvaka kukubaliana na ukweli huo kwani bado hakuweza kuamini kama Sabrina anaweza kulala na Jeff hadi kufikia hatua ya kuzaa naye.
Kwakweli ilikuwa ni ngumu sana kwa Sakina kukubaliana na hali halisi na kumfanya atamani usiku na mchana kumuuliza Sabrina ukweli wa mambo yote.

Jeff alikuwa ameenda stendi kumfata Aisha kwani alimtaarifu kuwa amefika na kweli alimkuta pale kituoni akimsubiria.
"Karibu sana Aisha, nilijua masikhara ujue"
"Yani ulijua natania Jeff? Hapana nilikuwa namaanisha kabisa"
"Basi sawa, karibu sana kwetu. Ila naomba nikuombe kitu"
"Niombe tu usijali Jeff"
"Pale nyumbani nitamwambia mama kuwa wewe ni mpenzi wangu kwahiyo usikatae tafadhari"
Aisha akatabasamu kwa furaha,
"Hilo sio tatizo Jeff yani sio tatizo kabisa hata usijali. Mi nitakubali chochote utakachosema"
Basi wakaanza kutembea taratibu kuelekea nyumbani kwakina Jeff.
Njiani wakaona gari ya Sam ikisimama mbele yao ambapo Sam alishusha kioo na kuwauliza wanapoelekea.
"Tunaenda nyumbani"
Jeff ndiye aliyejibu, kisha Sam akawaomba wapande kwenye gari ili awasogeze kidogo nao wakapanda.
Sam aliwapeleka hadi mlangoni kwakina Jeff ila kabla hawajashuka akauliza swali,
"Kumbe nyie mnafahamiana kiasi hiki hadi mnaenda nyumbani pamoja?"
Hapo ndio Aisha akadakia kujibu,
"Ndio, Jeff anaenda kunitambulisha kwao kama mke mtarajiwa"
Sam alibaki kushangaa na kuwaacha washuke, hata Jeff nae alimshangaa Aisha kwa jibu lake lililotolewa haraka haraka kiasi kile.
Kisha wakaingia ndani halafu Sam akaondoka zake.

Walimkuta sebleni mama yake na Jeff, ambapo Jeff alipoingia tu alianza kwa kumwambia mama yake,
"Mama, nimekuletea mgeni leo"
"Karibuni sana, ila kabla ya yote naomba umtambulishe tafadhari"
Jeff akatulia kimya kwa muda kwani akili yake ilikuwa kama inamzuia kwa kile anachotaka kusema na moyo wake nao ulikuwa unapingana na jambo lile.
Ila Aisha alipoona ukimya umetawala akaamua kuvunja ukimya huo kwa kusema,
"Mimi ndio mchumba wa Jeff mama"
Huku akitabasamu tu na kumfanya Sakina nae atabasamu ingawa kidogo amemshangaa huyu binti kwa kujitambulisha mwenyewe.
Ila akamkaribisha hivyo hivyo kwa ukarimu na furaha ingawa Jeff alikuwa kimya kabisa akimuangalia tu Aisha na kumfanya hadi mama yake amshtue.
"Vipi kwani una tatizo gani? Mbona kimya gafla?"
"Hapana tatizo mama, ila nilikuja nae huyu kwa lengo la kukusalimia tu mama angu. Ila naomba utupe ruhusa yako tuondoke mama"
"Kheee hata kukaa kidogo jamani! Mbona muondoke mapema hivyo? Subirini tule kwa pamoja tufurahi ndio muondoke"
"Hapana mama, kuna mahali tunataka kuwahi tafadhari mama"
"Hapana kwakweli, hapa mmefika na wala siwezi kuwaruhusu muondoke bila ya kupata baraka ya chakula cha pamoja. Ni haraka tu chakula kitakuwa tayari sababu nilishakibandika wanangu jamani"
Jeff hakuwa na la ziada, ikabidi tu atulie na kufata lile analosema mama yao.

Sam nae alifika kwakina Sabrina na kuwakuta mule ndani kisha akasalimiana nao kama kawaida na wao wakamkaribisha sana.
Pia akafurahi kumuona dada yake Joyce kwani ni kipindi kirefu hajaonana nae.
Muda kidogo akamuomba Sabrina na wakainuka kwenda kuongea kidogo,
"Naomba twende nyumbani Sabrina"
"Mmh hapana Sam, sipo tayari kurudi pale tena. Najua yule mzee atatusumbua tu, nawapenda wanangu Sam"
"Usijali, nishamaliza tatizo la yule mzee"
"Umelimalizaje?"
"Hata usijali Sabrina, wewe niamini kuwa lile tatizo limeisha na hata hivyo hatutaenda tena nyumba ile"
"Tutaenda wapi sasa?"
"Kuna nyumba nyingine nitawapeleka, huijui nyumba hiyo ila ndio itakuwa urithi wa watoto wangu"
Maneno haya ya urithi wa watoto yakamuingia akilini kidogo Sabrina kwani anajua wazi kuwa Sam hana mtoto yeyote isipokuwa  wale wawili tu ambao sio wake kwa kuzaa.
Sabrina akakubali ila kwa sharti kuwa nyumba hiyo isiwe kule kule kwa mwanzo yani iwe kweli, naye Sam akamuhakikishia na kumuomba akawaandae watoto.
Sabrina aliingia ndani na kumuacha Sam sebleni kisha yeye akaenda kuwaandaa wale watoto wao.
Muda kidogo akatoka na kuwaacha watoto sebleni halafu yeye akatoka nje, na moja kwa moja akaanza kuelekea kwakina Jeff kwani alihitaji awasindikize.

Sabrina alifika kwakina Jeff na moja kwa moja akaingia ndani kama kawaida yake, akawakuta wapo mezani wakila. Naje moja kwa moja akawafata eneo lile na kumshangaa Aisha pale.
Sakina alimkaribisha vizuri Sabrina,
"Karibu tule Sabrina, leo tumepata ugeni. Nimetembelewa na mchumba wa Jeff bhana anaitwa Aisha"
Jeff aliinama chini tu huku akimsikiliza mama yake akimaliza hoja zote kwa wakati mmoja.
"Usijali dada, nilikuwa na shida na Jeff kidogo ila kwavile unakula malizia basi halafu uje nyumbani, kuna kitu naomba ukanisaidie"
Kisha hakungoja jibu la yeyote kati yao na kuondoka.
Alirudi nyumbani kwao huku moyo ukimuuma sana.
Akamuona Sam akiwa nje ambapo alipomkaribia tu alimuuliza,
"Mbona umetoka nje?"
"Nilikuwa nakuangalia wewe, mbona uliondoka? Ulienda wapi?"
Akatafuta uongo wa haraka na kuukosa ikabidi tu amwambie ukweli kuwa alienda kumuita Jeff kuwa aje amsaidie baadhi ya vitu.
"Sasa yuko wapi?"
"Tuondoke tu kwanza mizigo yenyewe kidogo tu"
Sam akaelewa kabisa kuwa lazima Sabrina kamkuta Aisha kule ndiomana kamaindi ila akamkubalia na kuchukua begi mbili za nguo na kupakia kwenye gari kisha kuchukua watoto wote wawili ingawa mama yake aling'ang'ania kubaki na yule mkubwa ila Sabrina alimuahidi mama yake kumleta huyo mtoto kwa wakati mwingine kisha wakaondoka.
Ikabidi mama Sabrina amwombe James wamuachie yule mtoto wao wa kwanza japo kwa siku mbili tu,
"Mama jamani, ila tushamzoea chautundu wetu"
"Mwacheni bwana nikaekae nae kidogo"
Wakakubaliana juu ya hilo na wakakubali kumuachia mtoto huyo.

Sam alienda moja kwa moja na Sabrina kwenye nyumba mpya na kweli ilikuwa nzuri sana.
"Sasa siku zote alikuwa anakaa nani humu?"
"Hii nyumba haijawahi kukaliwa na mtu, ni mpya kweli. Kesho nitamleta huku yule mlinzi wa kule."
"Itakuwa vizuri"
"Ila usijali, binti wa usafi yupo anakuja asubuhi na kuondoka jioni"
Sabrina bado hakuelewa kuwa maandalizi ya ile nyumba yalianza lini.

Jeff alipomaliza kula tu alitoka pamoja na yule Aisha kisha wakamuaga mama yao.
Wakaelekea kwakina Sabrina pamoja kwani Aisha hakutaka kuachwa ndani tu.
Ila hawakumkuta Sabrina na kuambiwa kuwa ameondoka na mumewe.
Moja kwa moja akajua wamerudi tena kwao.
Akaamua kuaga pale na kuondoka huku akijiuliza kuwa kwanini Sabrina amewapeleka tena watoto wake wote kwenye ile nyumba ya mabalaa.
Akajikuta akisema kwa nguvu sasa,
"Anataka kunipotezea watoto yule"
Aisha akauliza,
"Watoto gani tena?"
Jeff akamgelesha pale kisha akamsindikiza Aisha na alipopanda gari tu naye akapanda kuelekea nyumbani kwa Sam.

Jeff alifika nyumbani kwa Sam, ila kabla hajasogelea geti akahisi kichwa chake kikiwa kizito sana na kumfanya afikirie kuwa kuna kitu.
Pale getini hakumkuta mlinzi wa Sam, ila geti lilionekana kurudishiwa tu.
Hivyobasi akaamua kulisukuma na kuingia ndani.
Akashangaa kumuona mlini wa Sam akiwa chini huku damu zikimtoka.

Itaendelea







USISAHAU KU LIKE PAGE YETU,BONYEZA LIKE BUTTON

No comments:

Theme images by pollux. Powered by Blogger.